Hospitali ya Taifa Muhimbili-Mloganzila imeendelea kujikita katika kuboresha huduma za matibabu ya kibingwa na ubingwa bobezi na kuweka rekodi ya kuwa hospitali ya kwanza nchini kufanya upasuaji wa kutengeneza mishipa ya kuchuja damu kwa wagonjwa wa figo kwa wakati mmoja, kwa kuwapatia matibabu hayo wagonjwa 41 hivyo kufikisha idadi ya wagonjwa 78 waliopatiwa huduma hiyo tangu ianze kutolewa mwaka 2023 hospitalini hapo.
Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili, Dkt. Delillah Kimambo amesema matibabu hayo yamefanyika katika kambi maalum ya siku tatu iliyofanyika hivi karibuni kwa kushirikiana na wataalam bobezi kutoka Korea Kusini pamoja na wataalamu wa ndani.
Aidha ameeleza kuwa kambi hiyo imeenda sambamba na huduma ya upandikizaji figo ambapo wagonjwa wanne wamenufaika na matibabu hayo na kufikisha idadi ya wagonjwa 19 ambao wamepandikizwa figo tangu huduma hiyo ilipoanza kutolewa hospitalini hapo mwaka 2023.
Kwa mujibu wa Dkt. Kimambo Muhimbili -Mloganzila ni hospitali pekee ambayo inatumia teknolojia ya kuvuna figo kutoka kwa mchangiaji kwa kutumia matundu madogo (Hand Assisted Donor Nephrectomy), teknolojia ambayo imekua rafiki kwa wachangiaji kwani hukaa wodini kwa muda mfupi na kurejea katika majukumu yao kwa haraka.


