WAZAZI na walezi wametakiwa kuwa na aina au mfumo wa malezi ya Kidemokrasia ikiwemo kujenga mahusiano mazuri pamoja na kutilia maanani hisia za mtoto au watoto.
Wito huo umetolewa leo Julai 3, 2024 katika Semina za Jinisa na Maendeleo ambazo hufanyika kila Jumatano katika Viwanja vya TGNP- Mtandao Mabibo Jijini Dar es Salaam.
Mwanasaikolojia Sylvia Sostenes wakati akiwasilisha mada kuhusu malezi, amewasihi walezi wote kuwa na muda wa kutosha wa kukaa na watoto wao kama nyenzo ya kufuatilia mwenendo wa mtoto au watoto.
Mwanasaikolojia
 huyo ameendelea kwa kufafanua kuwa, kulea ni pamoja na kuwekeza katika 
mahitaji muhimu kama lishe bora, afya ya mwili, roho na akili, elimu, 
ulinzi, muda kwa ajili ya kuchangamana na watoto.
Katika uwanda 
wa kisaikolojia, Bi. Sylvia ameeleza kuwa, malezi ni mchakato 
uliosheheni vitu vingi ndani yake lakini kubwa zaidi ikiwemo na kumpatia
 mtoto mahitaji yake na huduma muhimu. 
"Malezi ni mchakato wa 
maandalizi ya mtoto utakaomwezesha mtoto kukua, kukubalika, kujikubali, 
kushiriki katika shughuli za kijamii na kiutamaduni kwa kumlinda, 
kumjumuisha na kumpatia mahitaji na huduma za msingi" alisema Bi. Sylvia
 na kuongeza kuwa 
"Iwapo malezi ni mchakato wa maandalizi ya 
mtoto basi sharti iwepo mikakati toka kwa wazazi/walezi ili kufanikisha 
hili. Kwasasa tunaishi kwenye huu mtindo huria ambao ni wa kujipatia 
Watoto na kuwaacha wakue. Watoto wanajilea wao wenyewe."
Akichangia
 katika semina hiyo, Joseph Bulemo amesema kwa sasa, familia nyingi 
hazina ukaribu na watoto jambo linalopelekea matukio ya ukatili kwa 
watoto kuendelea kutokea.
Bw. Bulemo pia ameyataja malezi ya kimabavu dhidi ya watoto kama sababu inayopelekea watoto kuwa karibu na wazazi au walezi.
Naye
 Nantaika Maufi amashauri wazazi kuwa karibu na watoto katika kila hatua
 kwani kwa kufanya hivyo itawasaidia kugundua mapema mabadiliko yoyote 
au pindi watoto wapatapo changamoto yoyote au kufanyiwa ukatili huku 
akipinga hoja ya ugumu wa maisha na shughuli za utafutaji kama kikwazo 
cha kutokuwa karibu.
Kwa upande wake Mpegwa Noah amewataka wazazi
 na walezi kuwa na umoja wa dhati na uchungu sawa kwenye malezi kwa 
watoto wao, watoto wa majirani na watoto wengine wowote kwa kufanya 
hivyo itachangia watoto katika maadili mazuri kwa kuoata malezi bora.








 
 
 
 
 
 
 
 
