WARSHA Maalum kuhusu usalama wa  Mabwawa  ya tope sumu (Tailings Storage Facility (TSF) & mabwawa ya maji ya kawaida Water Dams imezinduliwa Leo Dodoma katika Ukumbi wa Midland Hotel mbele ya vyombo Vya Habari ikitazamiwa kuanza tarehe  28 hadi 30 Novemba 2023, Mjini Mwanza na kufuatiwa na mafunzo kwa vitendo yanayotarajiea kufanyika Bulyanhulu Gold Mine, Kahama.
Warsha hiyo ya kwanza kufanyika Tanzania inakwenda kusimamiwa na Taasisi ya Chemba ya Migodi Tanzania (TCM) pamoja na Wizara ya Maji (Chini ya Idara ya Mkurugenzi wa Rasilimali za Maji).
Akizungumza na Waaandishi wa Habari asubuhi ya Leo  Eng. Philbert Rweyemamu, Mwenyekiti wa Chemba ya Madini Tanzania
alisema Warsha hiyo ina kwenda  kuleta mabadiliko makubwa kiusalama.
Alisema.Chemba ya Madini na Wizara ya Maji wamejipanga Kuendesha Warsha hiyo inayolenga kuwaelimisha wadau kuhusu teknolojia za kisasa zilizopo na kuwapa uelewa wa pamoja na fursa ya  kuzungumza kuhusu ufuatiliaji wa usalama  wa Mabwawa hayo ya tope sumu (TSF) na Mabwawa ya maji ya kawaida.
Alisema usalama wa  Mabwawa hayo ni muhimu ili kuweza kuchukua hatua mapema kabla maafa hayajatokea.
"Tunaamini kuwa maarifa yatakayopatikana kutoka kwenye warsha hii yatawaongezea wasimamizi wa sheria na wamiliki wa mabwawa hayo uwezo  katika kusimamia usalama   hivyo kupunguza uwezekano wa kutokea ajali zinazoweza kuepukika" alisema Eng. Philbert Rweyemamu, Mwenyekiti TCM
Akieleza pia kuwa Tanzania inajivunia kuwa na baadhi ya Mabwawa ya tope sumu yalijojengwa kwa viwango vya kimataifa. Mabwa haya ni aliyataja kuwa ni pamoja na yale yaliyoko kwenye migodi ya  Geita Gold Mine, Bulyanhulu, North Mara, Buzwagi, Williamson Diamonds Mines, Stamigold, New Luika Gold Mine pamoja na Singida Gold Mine.
Pia kuna Mabwawa mengi ya Kuhifadhi Maji ambayo ni kwa ajili ya uzalishaji wa umeme wa maji, kama vile Bwawa la Maji la Mwalimu Nyerere, Nyumba ya Mungu, Kihansi, Mtera na mengine mengi bila kusahau Mabwawa mengine maarufu yanayotumika kuhifadhi maji, umwagiliaji na matumizi mbalimbali.
Akionyesha umuhinu wa warsha hiyo Eng Philbert Rweyemamu alisema  "Inapotokea Mabwawa haya yakapasuka, athari kubwa hutokea ikiwa ni pamoja na kuathiri shughuli za uzalishaji za kiuchumi, makazi, mashamba,  maisha ya binadamu, pamoja na  mazingira kwa ujumla."
TSF na Mabwawa ya maji ni miundo mbinu muhimu  katika sekta mbalimbali za kiuchumI lakini usalama wake  mara nyingi haupewi kipaumbele kulinganisha na maslahi ya kibiashara.
"Ni muhimu kusisitiza kwamba kuhakikisha usalama na  ubora wa Mabwawa haya ni jambo la msingi sana katika  kukuza uchumi endelevu. Zipo takwimu za kutisha za kimataifa kuhusu kupasuka kwa TSF na Mabwawa ya maji na kusababisha madhara makubwa ambazo  zinathibitisha ukubwa wa changamoto za mabwawa haya, hivyo   hatua za tahadhari  zinatakiwa kuchukuliwa haraka." Alisema na kutoa mfano kuwa
Hivi karibuni, mnamo Novemba 2022, Tanzania ilishuhudia ajali ya kupasuka kwa  TSF (Slimes dam)  kwenye  Mgodi wa Almasi wa Williamson Diamond Limited ulioko  huko Mwadui- Kishapu, mkoani Shinyanga,Ingawa hakuna madhara  makubwa yaliyotokea  lakini, karibu watu 130 walilazimika kuhamishwa na  matope kutoka kwenye bwawa yaliathiri  maeneo ya jirani, ikijumuisha Bwawa la Maji safi la New Alamasi, ambalo baadaye  ilibidi kutelekezwa.
Athari pia zilisababisha  hasara za kiuchumi, kwani uzalishaji katika Mgodi wa Mwadui ulisimama kwa takriban miezi  8 hadi ulipoanza  tena mwezi Julai 2023, na hivyo kusababisha  upotevu wa mapato kwa Serikali Kuu na Serikali za Mitaa, na pia kuathiri wafanyakazi karibu 1,000 na familia zao.
Alitoa mfano mwingine kuwa ni ule wa mwaka 2020, TSF ya North Mara ya Tarime ilikabiliwa na changamoto tofauti ya uhifadhi wa maji yenye sumu ambapo maji hayo yalivuja na kuathiri mazingira.  Uvujaji huu ulisababisha  uchafuzi wa maji ya chini ya ardhi, na kusababisha madhara kwa samaki na wanyama.
Aidha, mwaka   2016 mgodi wa dhahabu wa  eneo la Nyarugusu Mgodi uliopo Wilayani Geita nao ulipata hitilafu ya bwawa la tope sumu na kusababisha upotevu wa mali na uchafuzi mkubwa wa mazingira Matukio yaliyotajwa hapo juu yanasisitiza uharaka wa dhamira yetu ya pamoja ya kuimarisha usalama wa TSF na  usimamizi madhubuti wa mabwawa yote nchini Tanzania.
"Warsha hii inatoa fursa kwa wadau wote katika sekta ya madini na wale wa  usimamizi wa rasilimali za maji. Mafunzo haya yataenda mbali zaidi kukidhi matakwa ya sheria,  yatajikita pia kuangalia  vipengele muhimu vya usalama, udhibiti wa vihatarishi  kuhakiki usanifu wa mabwawa,  na taratibu za tahadhari za mapema.
Warsha hii itakuwa ni fursa ya  kukutana na wataalamu wabobezi katika utengezaji na matumizi ya vifaa vya kufuatilia usalama wa TSF na Mabwawa ya maji" aliyaongea hayo Eng Philbert Rweyemamu na kuwataja Wataalam hao kuwa wanatoka Kampuni ya OSIMO Technical (PTY) Limited  ya Afrika Kusini na pia kutoka nchiniHispania.Wataalam hao ambao ndio watatoa mada ni pamoja na Pro. Eben Rust  anayetoka Chuo Kikuu cha Pretoria akiwa na Kampuni ya  Osimo, akiwa na uzoefu wa  miaka 38.
Mwengine ni Pieter Horne, Mhandisi wa viwanda na mtaalam wa masuala ya kidigitali kwa muda wa mika 15 nchini Afrika Kusini. akitokea Kampuni ya OSIMO., Jose R. Garcia.- Pelayo anaetajwa kuwa na uzoefu wa zaidi ya miaka 8 katika masuala ya Geotechnical, Afya  na  Miundo mbinu pamoja na vifaa vya masuala ya mazingira,  Bwana Pelayo anatokea Hispania kwenye kampuni ya Ruspeco inayotoa suluhisho duniani kote katika masuala ya Geotechnics.
"Tunachukua Fursa hii kuwakaribisha wadau wote wanaohusika na usanifu, ujenzi, ukaguzi na ufuatiliaji wa usalama wa Mabwawa ya tope sumu pamoja na Mabwawa ya maji kushiriki katika Warsha hii muhimu ili tuweze kujadili kwa pamoja changamoto za Mabwawa haya na pia kujifunza teknolojia za kisasa zilizopo za kufuatilia usalama wa Mabwawa hayo." Alisema Eng Philbert Rweyemamu
Warsha  hii ni mahsusi kwa wadau Wafanyakazi wanaosimamia Mabwawa ya tope sumu migodini na wale wanaohusika na  Mabwawa ya maji, Wataalamu wa Usimamizi wa Mazingira .Maafisa Mazingira wa Wilaya kwenye maeneo yenye migodi mikubwa na ya kati; Wasimamizi wa sheria (Regulators) zinazohusu TSF na mabwawa wa maji, pamoja na Wataalamu Walioidhinishwa (APPs) kuhusiana na masuala yote ya TSF na Mabwawa ya maji.
Eng Philbert Rweyemamu alisema kuwa Warsha hii ni ya kwanza kufanyika Tanzania  na ni hatua muhimu kuelekea mustakabali endelevu zaidi wa sekta ya madini  na usimamizi wa rasilimali za maji nchini.
"Tunatazamia ushiriki na ushirikiano wa wadau wote"  :Eng. Philbert Rweyemamu,Mwenyekiti Tanzania Chember of Mines





 
 
 
 
 
 
 
