Breaking

Saturday, 21 May 2022

RAIS SAMIA KUFUNGUA MKUTANO WA MAKATIBU MAHSUSI DODOMA




Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam


RAIS Samia Suluhu Hassan, anaratajiwa kufungua Mkutano Mkuu wa Chama cha Makatibu Mahsusi Tanzania (TAPSEA) utakaofanyika mkoani Dodoma kuanzia Mei 31 hadi Juni 3 mwaka huu.


Hayo yamesemwa na Mwenyekiti wa TAPSEA, Zuhura Songambele wakati akizungumza na waandishi wa habari leo Jumamosi Mei 21, 2022 jijini Dar es Salaam, ambapo amesema pamoja na mkutano pia kutakuwa na uchaguzi mkuu Juni 3,2022.


Amesema mkutano huo mkuu unatarajiwa kukutanisha makatibu muhtasi na wadau wengine 4,000 kutoka kila kona ya nchi.


"TAPSEA ina wanachama 3,413 tunaamini watashiriki wote, ila kwa ujumla mkutano unaweza kukutanisha washiriki 4,000," amesema mwenyekiti.

Songambele amesema kuanzia Mei 31 na Juni mosi wanachama wa TAPSEA watapata fursa ya kujifunza mambo mbalimbali kuhusu sekta hiyo, hivyo kuwataka washiriki kwa wingi.


Amesema wamealika watoa mada mbalimbali ambao watatumia mkutano huo kuwapiga msasa wanachama wao.


"Tunapenda kutumia nafasi hii kuwakaribisha wana TAPSEA wote katika mkutano wetu unaotarajiwa kufunguliwa na Rais Samia. Nadhani wanaelewa kuwa jambo la mama ni jambo letu. Tuje kwa wingi kumsikiliza mama yetu naamini atajibu baadhi ya changamoto tunazopitia,"amesema.


Amesema Juni 3,2022 itakuwa siku ya mkutano mkuu na uchaguzi hivyo wana TAPSEA wote wanaruhusiwa kugombea, ili kupata viongozi wanawataka.


Songambele amesema katika uchaguzi huo nafasi zinazogombewa ni Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti, Katibu, Naibu Katibu, Mwekahazina na Wajumbe tisa.


Aidha, alitoa rai kwa viongozi wa Serikali na taasisi za umma kutoa ruhusa kwa makatibu muhtasi hao ili waweze kushiriki mkutano muhimu kwao.


Kwa upande mwingine Songambele amesema zipo baadhi ya changamoto wanakutana nazo ila wamekuwa wakizipatia ufumbuzi kwa wakati.


Mwisho.
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: +255 621 896 990

Pages